Leo ningependa tuangalie kidogo kuhusu vita ya kimawazo
Siku moja nikiwa nimelala, naliota ufalme wa Mungu na ule wa Shetani upo katika vita. Kila upande ulikuwa unafanya bidii kuhakikisha mawazo/matakwa yake yanatekelezwa kupitia mtu. Naam niliota kuna kitu Mungu anataka kizaliwe duniani kupitia mtu na Shetani naye akawa akipinga kile cha Mungu kwa kuleta cha kwake kizaliwe kupitia mtu huyo huyo. Baada ya kutafakari ndoto ile ndipo nikapata ujumbe huu, sasa endelea kujifunza.
Kwanza ni vizuri ukafahamu kwamba, ikiwa Mungu ana mawazo ya amani juu yako(Yeremia 29:11), basi, Shetani pia ana mawazo ya uharibifu juu yako. Na hii ina maana kila siku mwanadamu atakutana na vita ya nini atekeleze katika ufahamu wake, naam hii ndiyo vita ya mawazo. Mungu atapigana kuhakikisha mawazo yake juu yako yanafanikiwa na Shetani naye atapigana kuhakikisha mawazo yake kupitia wewe yanafanikiwa.
Kumbuka kwamba Mungu anapotaka kufanya jambo lolote chini ya jua anatumia njia ya kuweka wazo ndani ya mtu. Wakati huo huo Shetani naye akijua kwamba wazo la Mungu litaleta uharibifu kwenye ufalme wake, atahakikisha analeta wazo lake, kwa lengo la kuondoa wazo la Mungu ndani yako, ili kuleta uharibifu kwenye ufalme wa Mungu.
Jambo hili ndilo lilitokea kwa Adam na Eva pale bustanini, Shetani alipoleta wazo la uharibifu kwenye ufahamu wa Eva na kisha Eva akakubaliana na lile wazo la uharibifu, akawa ameharibu mpango wa Mungu juu ya maisha yao. Naam nafsi/akili ya mtu ni kiungo au uwanja wa vita vya mawazo ya upande wa Mungu na upande wa Shetani.
Kumbuka kwamba Vita vya kiroho, ni vita ambayo inapigwa katika ulimwengu wa roho, kwa jinsi ya rohoni baina ya ufalme wa Mungu na wa Shetani kupitia watendaji wao kwa lengo la kumpata mwanadamu, ili kila ufalme umtumie kutekeleza au kufanikisha makusudi yake ya ulimwengu wa roho kwenye ulimwengu wa mwili ambao mwanadamu mwenye mwili wa damu na nyama anaishi.
Vita vya kiroho ni kile ambacho mimi nakiita vita ya matakwa (a war of wills). Kila ufalme katika ulimwengu wa roho, una mambo yake ambayo unataka kuhakikisha yanatimia katika ulimwengu wa mwili, naam ulimwengu ambao roho yenye mwili ndio inayotawala. Viumbe walioko kwenye ulimwengu wa roho hawana mwili wa damu na nyama kama vile sisi tulivyo. Kwa hiyo wanapotaka kutawala kwenye ulimwengu huu, hawana namna ya kufanya zaidi ya kumtumia mwanadamu.
Kwa hiyo mwanadamu anakuwa kiungo muhimu sana kati ya ulimwengu wa roho na huu wa mwili. Na kwa sababu hiyo kila ufalme unafanya jitihada ya kuhakikisha unachukua utawala kwenye nafsi ya mwanadamu ili umtumie kwa kazi yake hapa duniani. Naam huo ndio mwanzo wa vita vya kiroho kati ya Mungu na Shetani, nia yao ikiwa ni kuhakikisha matakwa yao yanafanikiwa kupitia mtu. Na ndio maana, kwa Mungu, mtu ni wa muhimu sana (Zaburi 8:4-8).
Na kwa sababu hii unapaswa kuwa makini kwa habari ya nini unairuhusu nafsi yako ikitafakari, ukijua kwamba vita kubwa ya Mungu na Shetani ni kuwa na utwala wa nafsi yako ili kuongoza mawazo yako na maamuzi yako. Fahamu kwamba Mungu akiongoza nafsi yako ataongoza maamuzi yako pia. Vivyo Shetani akikamata nafsi yako amekamata maamuzi yako na future yako. Hivyo hakikisha unaenenda kwa roho na kuyatafakari mambo ya rohoni ili kuyafanya mapenzi ya Mungu ukikumbuka kwamba siku zote yeye anakuwazia mawazo ya amani.
Bwana Mungu akubariki na akupe ushindi katika kila vita ya mawazo unayoikabili.
Advertisements
Comments
Post a Comment
asante kwa kuichagua tujengane media kuwa sehemu yako ya kujifunza