Skip to main content

MSAADA UTOKAO KWA MUNGU JUU NA ALIYE HAI


MIAKA 2,000 hivi iliyopita, Paulo, mwandikaji wa Biblia alimfafanua Yehova kuwa “Mungu anayetoa uvumilivu na faraja.” (Waroma 15:5) Kwa kuwa Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova habadiliki kadiri wakati unavyopita, tunaweza kuwa na hakika kwamba bado Mungu anawafariji wale wanaomtumikia. (Yakobo 1:17) Kwa kweli, Biblia inafunua kwamba Yehova anawafariji kwa njia mbalimbali wale walio na uhitaji. Ni njia gani hizo? Mungu anawatia nguvu wale wanaomwomba msaada kupitia sala. Pia, Mungu anawachochea Wakristo wa kweli kuwafariji waamini wenzao. Na Yehova ameweka katika Neno lake, Biblia, masimulizi yenye kutia moyo ambayo yanawatia nguvu hasa wale wanaoomboleza kifo cha mtoto. Acheni tuchunguze aina hizo tatu za faraja, moja baada ya nyingine.“Yehova Mwenyewe Akasikia”Mfalme Daudi aliandika hivi kuhusu Muumba wetu, Yehova: “Mtegemeeni nyakati zote. Mimineni moyo wenu mbele zake. Mungu ni kimbilio letu.” (Zaburi 62:8) Kwa nini Daudi alikuwa na uhakika huo katika Yehova? Daudi aliandika hivi kujihusu: “Huyu mwenye kuteseka aliita, na Yehova mwenyewe akasikia. Na Yeye akamwokoa kutoka katika taabu zake zote.” (Zaburi 34:6) Katika taabu zote zilizompata maishani, sikuzote Daudi alimwomba Mungu msaada, na sikuzote Yehova alimsaidia. Daudi alijua kutokana na mambo yaliyompata kwamba Mungu angemtegemeza na kumsaidia kuvumilia.Wazazi wanaoomboleza wanahitaji kujua kwamba Yehova atawategemeza wakati wa huzuni nyingi, kama tu alivyomtegemeza Daudi. Wanaweza kumkaribia ‘Msikiaji mkuu wa sala,’ wakiwa na hakika kwamba atawasaidia. (Zaburi 65:2) William, aliyetajwa katika habari iliyotangulia, alisema hivi: “Mara nyingi, nimehisi kwamba singeweza kuvumilia kuishi tena bila mwana wangu, na nimemwomba Yehova anitulize. Sikuzote amenipa nguvu na uhodari wa kuendelea kuishi.” Wewe pia ukisali kwa Yehova kwa imani, Mungu mkuu wa mbinguni atakutegemeza. Mwishowe, Yehova Mungu anawaahidi hivi wale wanaojitahidi kumtumikia: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”—Isaya 41:13.Msaada Kutoka kwa Marafiki wa KweliWale waliofiwa na mtoto mara nyingi wanahitaji wakati wa kuomboleza na kukabiliana na hisia zao wakiwa peke yao. Hata hivyo, halingekuwa jambo la hekima kwao kujitenga na wengine kwa muda mrefu. Kulingana na Methali 18:1, “mtu anayejitenga” anaweza kuumia. Kwa hiyo, wale wanaoomboleza wanapaswa kuwa waangalifu wasianguke katika mtego wa kujitenga.Marafiki wanaomwogopa Mungu wanaweza kuwasaidia sana wale wanaotaabika. Andiko la Methali 17:17 linasema hivi: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” Lucy, ambaye pia alitajwa katika habari iliyotangulia, alifarijiwa na marafiki wa kweli baada ya kufiwa na mwana wake. Alisema hivi kuhusu waamini wenzake kutanikoni: “Walitusaidia sana walipotutembelea, hata ingawa nyakati nyingine walisema machache. Rafiki mmoja alinitembelea siku ambazo nilikuwa peke yangu. Alijua kwamba ningekuwa nyumbani nikilia, na mara nyingi alikuja na kulia pamoja nami. Mwingine alinipigia simu kila siku ili kunitia moyo. Wengine walitualika nyumbani kwao kwa ajili ya chakula, na waliendelea kufanya hivyo.”Ingawa uchungu mwingi ambao wazazi wanahisi wanapofiwa na mtoto hautoweki kwa urahisi, kusali kwa Mungu na kushirikiana na marafiki Wakristo kunaweza kuleta faraja ya kweli kwa wale wanaoomboleza. Wazazi wengi Wakristo ambao wamefiwa na mtoto wanatambua kwamba Yehova yuko pamoja nao. Ndiyo, Yehova “anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.”—Zaburi 147:3.Masimulizi ya Biblia YanayofarijiZaidi ya sala na ushirika unaojenga, Neno la Mungu lililoandikwa ni chanzo cha faraja kwa wale wanaoomboleza. Masimulizi ya Biblia yanaonyesha kwamba Yesu anatamani sana na ana uwezo wa kuondoa uchungu wa wazazi waliofiwa kwa kuwafufua wafu. Masimulizi kama hayo yanawafariji kikweli wale wanaoomboleza. Acheni tuchunguze masimulizi mawili kama hayo.Luka sura ya 7 inaeleza jambo lililotukia Yesu alipokutana na msafara wa mazishi katika jiji la Naini. Watu hao walikuwa karibu kumzika mwana pekee wa mjane. Mstari wa 13 unasema hivi: “Bwana alipomwona akamsikitikia, akamwambia: ‘Acha kulia.’”Ni watu wachache sana wanaoweza kuthubutu kumwambia mama aache kulia katika mazishi ya mwana wake. Kwa nini Yesu alisema hivyo? Kwa sababu alijua kwamba huzuni ya mama huyo ilikuwa karibu kutoweka. Simulizi hilo linaendelea kusema hivi: “[Yesu] akakaribia na kuligusa sanduku, na wachukuzi wakasimama tuli, naye akasema: ‘Kijana, ninakuambia, Inuka!’ Na huyo mfu akaketi na kuanza kusema, naye akamkabidhi kwa mama yake.” (Luka 7:14, 15) Wakati huohuo, haikosi mama huyo alilia tena, lakini wakati huu alilia kwa sababu ya furaha.Pindi nyingine, Yesu alifikiwa na mwanamume aliyeitwa Yairo, ambaye aliomba msaada kwa ajili ya binti yake mwenye umri wa miaka 12 aliyekuwa mgonjwa sana. Muda mfupi baadaye, Yairo alijulishwa kwamba binti yake alikuwa amekufa. Habari hizo zilimvunja moyo Yairo, lakini Yesu alimwambia hivi: “Usiogope, uwe tu na imani.” Yesu alienda katika nyumba ya familia hiyo ambamo msichana huyo aliyekufa alikuwamo. Yesu alisema hivi huku akimshika mkono: “Mwanamwali, ninakuambia, Simama!” Kulitukia nini? “Mara yule mwanamwali akasimama akaanza kutembea.” Wazazi wake walihisi namna gani? “Wakawa na shangwe kubwa.” Yairo na mke wake walimkumbatia binti yao, nao wakafurahi sana. Ni kana kwamba walikuwa wakiota ndoto.—Marko 5:22-24, 35-43.Masimulizi kama hayo ya Biblia yanayoeleza mambo waziwazi kuhusu ufufuo wa watoto yanawaonyesha wazazi wanaoomboleza mambo wanayoweza kutazamia wakati ujao. Yesu alisema: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Yehova anakusudia Mwana wake awape wafu uhai. Mamilioni ya watoto waliokufa “wataisikia sauti yake” anapowaambia hivi: ‘Ninawaambia, Simameni!’ Watoto hao wataanza tena kuzungumza na kutembea. Na kama Yairo na mke wake, wazazi wa watoto hao ‘watakuwa na shangwe kubwa.’Ikiwa umefiwa na mwana au binti yako, tafadhali jua kwamba Yehova anaweza kugeuza huzuni yako iwe shangwe kupitia ufufuo. Ili ufaidike na tumaini hilo tukufu, tii himizo hili la mtunga-zaburi: “Mtafuteni Yehova na nguvu zake. Utafuteni uso wake daima. Kumbukeni kazi zake za ajabu ambazo amefanya, miujiza yake.” (Zaburi 105:4, 5) Ndiyo, mtumikie Mungu wa kweli, Yehova, na umwabudu kwa njia anayokubali.Utapata faida gani sasa ‘ukimtafuta Yehova’? Utatiwa nguvu ukisali kwa Mungu, utafarijiwa na hangaiko lenye upendo la marafiki wa kweli Wakristo, na utatiwa moyo ukijifunza Neno la Mungu. Zaidi ya hayo, hivi karibuni, utaona ‘kazi za ajabu na miuujiza’ ambayo Yehova atatimiza kwa faida yako ya milele na faida ya mtoto wako ambaye amekufa.[Sanduku katika ukurasa wa 5]“Mlete Yule Mwanamke Aliyefiwa na Watoto Wawili”Kehinde na Bintu, wenzi wa ndoa nchini Nigeria ambao ni Mashahidi wa Yehova walifiwa na watoto wao wawili katika msiba wa gari. Tangu wakati huo, wamehisi uchungu kwa sababu ya msiba huo mbaya. Hata hivyo, kumtumaini Yehova kunawategemeza, na wanaendelea kuwatangazia majirani wao ujumbe wa Biblia unaotoa tumaini.Wengine walitambua kwamba Kehinde na Bintu walikuwa watulivu na wenye nguvu. Siku moja mwanamke anayeitwa Bi. Ukoli alimwambia hivi mmoja wa marafiki wa Bintu: “Mlete yule mwanamke aliyefiwa na watoto wawili wakati mmoja na ambaye bado anahubiri ujumbe wa Biblia. Ningependa kujua ni nini kinachompa nguvu za kuvumilia.” Bintu alipofika nyumbani kwa mwanamke huyo, Bi. Ukoli alimwambia hivi: “Ninataka kujua kwa nini bado unahubiri kuhusu Mungu aliyewaua watoto wako. Mungu alimchukua binti yangu wa pekee. Tangu wakati huo, sipendezwi na mambo ya Mungu.” Bintu alitumia Biblia kueleza sababu inayofanya watu wafe na kwa nini tunaweza kuwa na tumaini hakika kwamba wapendwa wetu waliokufa watafufuliwa.—Matendo 24:15; Waroma 5:12.Baadaye, Bi. Ukoli alisema: “Nilikuwa nikifikiri kwamba Mungu ndiye anayewaua watu. Sasa ninajua ukweli.” Aliamua kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova ili ajifunze mengi zaidi kuhusu ahadi za Mungu.(‘Ninataka Kusaidia, lakini Sijui Jinsi ya Kufanya Hivyo’)Ingawa wazazi, ndugu, na dada za mtoto aliyekufa wanahuzunika sana, huenda marafiki wakawa na wasiwasi. Wanataka kuitegemeza familia hiyo lakini wanaogopa kwamba watasema au kufanya jambo litakalowaumiza hata zaidi. Yafuatayo ni mapendekezo fulani kwa ajili ya wale ambao huenda wakasema, ‘Ninataka kusaidia, lakini sijui jinsi ya kufanya hivyo.’
❖ Usiwaepuka watu waliofiwa eti kwa sababu hujui useme au ufanye nini. Utawatia nguvu kwa kuwa tu pamoja nao. Je, unashindwa useme nini? Kuwakumbatia na kusema kwa unyofu “Poleni sana,” kutawafanya watambue kwamba unawajali. Je, unaogopa kwamba ukianza kulia utafanya wahuzunike zaidi? Biblia inasema hivi: “Lieni pamoja na watu wanaolia.” (Waroma 12:15) Machozi yako yanaonyesha kwamba unahuzunika pamoja nao, na hilo linafariji.
❖ Chukua hatua ya kwanza. Je, unaweza kutayarishia familia hiyo chakula kidogo? Je, unaweza kusafisha vyombo walivyotumia? Je, unaweza kwenda kuwafanyia shughuli mbalimbali? Usiseme, “Mnaweza kunijulisha ikiwa mnahitaji chochote.” Hata ukisema maneno hayo kwa unyofu, wazazi wengi waliofiwa wataelewa kwamba huwezi kuwasaidia kwa sababu una shughuli nyingi. Badala yake, uliza “Ninaweza kuwasaidia jinsi gani sasa?” na kisha utimize ombi lao. Lakini epuka kuingia sehemu za faragha nyumbani mwao au kuingilia mambo yao ya kibinafsi.
❖ Epuka kusema, “Ninajua jinsi mnavyohisi.” Kila mwanadamu anakuwa na hisia tofauti kuelekea kifo cha mpendwa wake. Hata ikiwa wewe pia umefiwa na mtoto, hujui kwa uhakika jinsi wanavyohisi.
❖ Muda mrefu utapita kabla ya familia hiyo kurudia hali yake ya kawaida. Endelea kusaidia kadiri unavyoweza. Mwanzoni, watu wengi wanaishughulikia familia iliyofiwa, lakini familia hiyo inahitaji mengi zaidi. Uwe macho kuona mahitaji yao katika majuma na miezi itakayofuata.*

Comments

Popular posts from this blog

MAMBO YA KUZINGATIA WAKATI WA UCHUMBA

Yafuatayo ni mambo ya msingi kufanya katika kipindi cha uchumba; Jambo la kwanza –    Mruhusu Roho Mtakatifu afanyike Bwana wa uchumba wenu 2Wakorinto 3:17  ‘Basi Bwana’ ndiye Roho; na alipo Roho wa Bwana, hapo ndipo penye uhuru’. Kumbuka Roho Mtakatifu ni msaidizi. Hivyo basi ni vema kumtumia vema hasa katika nyanja hii ya mahusiano katika kipindi hiki cha uchumba. Ni Roho Mtakatifu pekee mwenye uwezo wa kukujulisha mambo na siri nyingi kuhusu mchumba wako hata kama yeye hataki kukueleza. Ukimruhusu Roho Mtakatifu afanyike Bwana, yeye atakuongoza katIka kufanya maombi yanayolenga maeneo ya msingi juu ya huyo mwenzako. Kila mtu ameumbwa pamoja na mapungufu fulani au kwa lugha nyingine mapungufu/ udhaifu (weakness) ni sehemu ya maisha ya mwanadamu. Roho Mtakatifu anapokuwa Bwana wa mahusiano yako yeye atakusaidia kuona madhaifu au mapungufu ya mwenzako kama kitu cha wewe kujivunia(Strength) kwa maana ya kuona udhaifu wa mwenzako kama kitu chema na si kibaya. Kum...

VITU VYA MSINGI VINAVYOWEZA KUKUSAIDIA KUDUMISHA UPENDO KATIKA MAHUSIANO

Kuna nukuu inayosema “Uhusiano mzuri hautokei tu peke yake bali huchukua muda, uvumilivu, na watu wawili ambao kikweli wanataka kuwa pamoja.” Japo inasemwa kuwa mapenzi hayana njia moja ya kufuatwa lakini kuna vitu ambavyo vinajulikana kuchangia katika kuboresha mahusiano baina ya wapenzi. Mahusiano ya mapenzi yenye kudumu ni sharti yapandwe katika udongo wenye rutuba kama ulivyo mmea, yatahitaji maji ya kumwagilia na mbolea ya kukuzia.  Na zaidi ya yote yanahitaji muda wa kukua kabla matunda kuonekana. 1. Uaminifu Kumwamini mwenza wako ni jambo la msingi sana katika kudumisha mahusiano. Usimshuku mpenzi wako kuwa si muaminifu bila ushahidi wowote. Kushukiwa kukosa uaminifu pasipo ukweli inasononesha sana na kumkosesha raha mpenzi wako. Imesemwa na wanafalsafa wa mawazo ya binadamu kuwa “Unachofikiri na kuamini kinatokea” hivyo unashauriwa kutofikiri vibaya juu ya mpenzi wako kwani haileti afya katika mahusiano. Hali kadhalika na wewe uwe mwaminifu na mwenye kusema kweli...

ZINGATIA HAYA UNAPOKUWA MBALI NA MWENZI WAKO

KAMA UKO MBALI NA MPENZI WAKO ZINGATIA HAYA Kama unaishi mbali na mpenzi wako kwanza kabisa unatakiwa kukubali kua mko mbali, huwezi na wala hutakiwi kucontrol kile anachokifanya kule, acha kufuatilia anafanya nini huko, yuko na nani na mambo kama hayo, kwa kfuupi wivu weka pembeni kwani ukiendekeza utachanganyikiwa. Kuna mambo mengi atayafanya mazuri na mabaya lakini kama hakuonyeshei basi huna haja ya kuyafukunyua. Jambo la pili ni mawasiliano haya ni muhimu na anapokupigia simu au unapompigia tumieni muda wenu vizuri kwa kuongelea kuhusu mapenzi na si kila siku “Mbona hukupokea simu yangu? Mbona nilikuona online hukujibu SMS zangu? Kulalamika sijui nimesikia hivi? Nimesikia vile!” Atakuvumilia kwa muda kisha itaboa na atakua anakwepa kuzungumza nawe na mwisho mapenzi yatakufa. Hata kama mnaongea dakika tano zifanyeni ziwe tamu zihusu mapenzi na si kuzozana mpaka mtu akitaka kupiga simu anawaza hivi nikiongea naye si kelele tu, hakuna mtu anapenda kupigia simu mtu aliyenuna....